-->

Header Ads

Jinsi mume alivyomuua mke kwa risasi na yeye kujiua




Mtoto Ester Maxmilian (17) ameelezea vifo vya wazazi wake waliofariki baada ya baba yake kumpiga risasi mama na yeye kujipiga risasi.

Wawili  hao ni Maxmilian Tula (40) aliyejipiga risasi kifuani baada ya kumpiga risasi tatu mkewe Teddy Malulu (38) huku chanzo vifo hivyo kikiwa na utata.

Wanandoa hao wamezaa watoto wawili, Ester na Grace Maxmilian huku mwanamume akidaiwa kuwa watoto wengine wawili Faith na Fero aliozaa na mwanamke mwingine nje ya ndoa.

Akisimulia mkasa huo nyumbani kwao mtaa wa Kanyerere Kata ya Mahina wilayani Nyamagana jijini Mwanza, mtoto huyo amesema ugomvi wa wazazi wake ambao ulidumu kwa takriban saa moja ulianza baada ya mama yake kurudi nyumbani saa 5.00 usiku akiwa amelewa na kumkuta baba yake  ambaye alirejea nyumbani tangu saa 3.00

Hata hivyo amesema baba na mama yake wamekuwa wakigombana lakini siku hiyo ilikuwa tofauti.

“…Sisi tulikuwa chumbani kwetu tumelala na wao wakawa wanazozana na kutufuata chumbani kwetu.”

Amesema kuwa wakati wa majibizano hayo mama alikuwa akitoa maneno machafu kwa baba, kisha wakaondoka kwenda chumbani kwao.

“Ila baba akamwambia mama kuwa wewe kila siku unanifanyia hivi ila leo ni mwisho, baadaye tulisikia mama akiaza kulalamika akidai kuwa utaniua na kuomba msamaha baba anakataa.”

“Baada ya muda tulisikia risasi tatu zimefyetuliwa, tena tukasikia risasi nyingine ya nne ndipo tulipoenda chumbani tulikuta mama anagaragara chumbani akisema mwangalieni baba yenu amejiua kwa risasi na mimi mnipeleke hospitali, alikuwa amepigwa risasi begani, paja na tumboni.” alisema Ester

Mwenyekiti wa mtaa huo, William Ngongo amesema mwanamke huyo alipelekwa hospitali ya rufaa ya Bugando na saa 1.00  asubuhi walipata taarifa kuwa amefariki dunia ila mwanamume alifia palepale tukio hilo ni kwanza kutokea.

Kamanda wa polisi mkoani Mwanza, Ahmed Msangi amesema chanzo cha tukio hilo kinachunguzwa.




JIUNGE NASI AKISI TV KILA SIKU KUPATA HABARI ZA UHAKIKA Nini maoni yako? Weka comment yako hapa,

No comments

Powered by Blogger.