-->

Header Ads

Rais mpya Somalia aapishwa, aahidi kurejesha heshima ya taifa hilo

Rais mpya wa Somalia, Mohamed Abdullahi Mohamed Farmajo ameapishwa leo mjini Mogadishu katika sherehe iliyohudhuriwa na viongozi wa nchi kadhaa za kanda hiyo chini ya hatua kali za ulinzi.
Baada ya kuapishwa Rais mpya wa Somalia ameahidi kurejesha heshima ya nchi hiyo ya Pembe ya Afrika lakini pia ameonya kwamba, itachukua miongo miwili kurekebisha nchi hiyo.
Amesema Somalia inakabiliwa na changamoto nyingi na kwamba mafanikio ya serikali yake yatakuwa madogo kutokana na rasilimali zake chache.
Mohamed Farmajo amesema Somalia imekuwa katika vita kwa kipindi cha miaka 26 iliyopita ikisumbuliwa na migogoro na ukame na kwa msingi huo itachukua miaka 20 kurekebisha nchi hiyo.

Amesema kizingiti kikubwa zaidi cha Somalia ni ukosefu wa amani na ukame uliowaathiri mamilioni ya raia na kwamba serikali yake itayapa umuhimu na mazingatio zaidi masuala ya maridhiano ya kitaifa, uadilifu na utawala wa sheria na vilevile kurejesha imani ya wananchi kwa serikali yao. Vilevile ameahidi kupambana na ufisadi katika nchi hiyo ambayo shirika la Transparency International limeitaja kuwa ndiyo inayoongoza duniani katika rushwa na ufisadi.
Rais Mohamed Abdullahi Farmajo alichaguliwa mapema mwezi huu katika hatua ya kuelekea kwenye serikali kuu ya kwanza nchini Somalia katika kipindi cha robo karne iliyopita.        

No comments

Powered by Blogger.