-->

Header Ads

Rais Magufuli awasilisha fomu inayotaja mali na madeni yake


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 28 Desemba, 2017 amewasilisha fomu yake ya tamko kuhusu rasilimali na madeni katika ofisi ya Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma iliyopo Mtaa wa Ohio, Wilaya ya Ilala Jijini Dar es Salaam.

Baada ya kuwasilisha fomu hiyo Mhe. Rais Magufuli ameipongeza Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa kazi inazofanya na amemtaka Kamishna wa Maadili Jaji Mstaafu Harold Nsekela kutopokea fomu ya kiongozi yeyote ambaye atakuwa hajawasilisha tamko lake ifikapo tarehe 31 Desemba, 2017.

“Mhe. Jaji Nsekela ikifika tarehe 31 Desemba, ambayo ni siku ya mwisho kwa Mujibu wa Sheria, weka mstari na usipokee fomu zingine, halafu tuone sheria itafanyaje, nakutakia kazi njema” amesisistiza Mhe. Rais Magufuli.

Kwa upande wake Mhe. Jaji Mstaafu Harold Nsekela amemshukuru na kumpongeza Mhe. Rais Magufuli kwa kutekeleza matakwa ya kisheria yanayomlazimu kujaza fomu hizo na amesisitiza kuwa ujazaji wa fomu hizo kwa viongozi wa umma sio ombi.

“Viongozi hawaombwi kujaza fomu hizi, kuna baadhi wanadhani labda kutuletea hilo tamko ni fadhila, hapana, sheria ya nchi inahitaji hivyo na kuna sababu zake za msingi” amesema Mhe. Jaji Mstaafu Nsekela.

Aidha, Mhe. Jaji Mstaafu Nsekela amempongeza Mhe. Rais Magufuli kwa kuwasilisha taarifa ya akaunti yake ya benki sambamba na tamko hilo, na amekiri kuwa ameonesha mfano wa kuigwa na viongozi wengine.

Tamko la viongozi wa umma kuhusu rasilimali na madeni linatolewa kwa mujibu wa kifungu cha 9 na cha 11 cha sheria ya maadili ya viongozi wa umma namba 13 ya mwaka 1995

Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
28 Desemba, 2017

No comments

Powered by Blogger.